MASTAA wanaotikisa kunako Bongo Movie, Steve Nyerere pamoja na Juma Chikoka leo wametinga ndani ya Ofisi za Global Publishers zilizopo Bamaga-Mwenge jijini Dar kwa nyakati tofauti wote huku ujio wao ukilenga katika siasa.
Akizungumza na waandishi wa habari kupitia Global TV Online, Steve Nyerere aliuelezea ujio wake kuwa yupo mbioni kutangaza nia ya kulichukua Jimbo la Kinondoni linaloshikiliwa na Mhe. Idd Azzan.
"Nimeamua na niko njiani kulichukua Jimbo la Kinondoni kupitia Chama cha Mapinduzi hivyo basi hivi karibuni waandishi wote wa habari nitakuwa nao ndani ya Viwanja vya Biafra, Kinondoni jijini Dar kutangaza nia. Hii haitaitwa safari ya matumani bali kijana ukimpa nafasi anaweza," alisema Steve.
Naye staa wa filamu Bongo, Juma Chikoka aliuzungumzia ujio wake kuwa amefurahishwa na Chama cha Mapinduzi kumpa cheo cha kuwa mhamasishaji wa vijana ngazi ya taifa.
"Aprili 18 mwaka huu niliitwa na CCM na wakaniambia kuwa wananihitaji katika kuhamasisha vijana kitaifa ambapo kazi hiyo nimeitekeleza kwa mkono mmoja. Si kwamba nitaacha kujihusisha na filamu bali wakinihitaji huko nitakuwepo na niko tayari," alisema Chikoka.